Monday, September 19, 2011

Maombi Peke Yake Bila Imani Hayatoshi Kutengeneza Jibu La Mahitaji Yako.

Marko 9:14-29.

Hii ni habari ya yule baba aliyekuwa na mwana mwenye pepo bubu na kiziwi, akamleta kwa wanafunzi wasiweze kumtoa. Wakati huo Yesu alikuwa mlimani akiomba na wanafunzi wengine watatu, aliposhuka baba mwenye mtoto akamwambia, Mwalimu nimemleta mwanangu kwako , ana pepo bubu, na kila ampagaapo humbwaga chini , naye hutoka povu na kusaga meno na kukonda , nikasema na wanafunzi wako wamtoe pepo wasiweze, akawajibu akasema enyi kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Nichukuliane nanyi hata lini? Mleteni kwangu akamponya.


Ukisoma ule mstari  wa 28 Biblia inasema “ Hata alipongia nyumbani, wanafunzi wake wakamwuliza, mbona sisi hatukuweza kumtoa? Akawaambia namna hii haiwezi kutoka kwa neno lolote , isipokuwa kwa kuomba.

Mpenzi msomaji ni vema nikushirikishe mojawapo ya siri nyingi za ajabu katika fungu hili la maneno, nayo ni ‘Maombi peke yake bila imani hayatoshi kutengeneza jibu la mahitaji yako’.

Katika habari hii, huyu baba alimleta mwanawe kwa Yesu ili amponye, sasa kwa bahati nzuri hakumkuta Yesu bali   wanafunzi tisa na watu wengine. Nasema kwa bahati nzuri kwa sababu Yesu angekuwepo huenda tusingejifunza kutokana na makosa ya wanafunzi wale tisa.

Wale wanafunzi walijaribu kumuombea yule kijana mgonjwa lakini wakashindwa kumtoa yule pepo. Yesu alipowasili na kupewa taarifa hizo aliumia sana akawauliza enyi kizazi kisicho amini nikae nanyi hata lini, kwa lugha rahisi alikuwa akiwaambia kukosa kwenu imani kumesababisha mshindwe kutoa huyu pepo na si kitu kingine.

Sasa swali walilomuuliza Yesu kwenye mstari wa 28 linaonyesha wanafunzi hawakuelewa kwa nini wao walishindwa kumtoa pepo? Ndipo Yesu akawajibu namna hii haiwezi kutoka kwa neno lolote, isipokuwa kwa kuomba.

Ukiliangalia jibu la Yesu si rahisi sana kumuelewa. Unaweza kufikiri aliwachanganya zaidi wanfunzii kwa jibu lake. Kwa sababu aliposema namna hii haitoki isipokuwa kwa kuomba alimaanisha nini? Je ina maana wanafunzi walikuwa hawaoombi? Kwa vyovyote vile walikuwa wanaomba, Je nini kilipungua kwenye maombi yao? Mstari wa 19 unatoa jibu pale aliposema enyi  kizazi kisichoamini, nikae nanyi hata lini? Na hapa ndipo tunapojua kumbe maombi peke yake bila imani hayatoshi kutengeneza jibu la mahitaji yatu.

Imani ni nini? Waebrania 11:1 inajibu “ Imani ni kuwa na uhakika wa mambo yatarijiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana”. Ule mstai wa sita pia unasema “Lakini pasipo imani haiwezekani kumpendeza , kwa maana mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao”.



Kitu gani tunajifunza hapa? wakati wanafunzi wanaomba ndani yao walikosa uhakika wa mambo yatarijiwayo, kwa lugha rahisi maombi yo yalikosa au kupungukiwa imani, yaani ndani yao uhakika wa yule pepo kutoka haukuwepo wakati wanaomba.
Neno linasema kila amwendeaye/aombaye lazima aamini kwamba yeye yupo.
Hivyo wanafunzi walitakiwa kuomba + imani = jibu la hitaji la yule baba.
Au walitakiwa kuomba/kukemea/kutaja hitaji lao + uhakika kwamba yule pepo atatoka = Pepo kutoka na kijana kufunguliwa.

Mpenzi msomaji nimalize kwa kusema hata wewe najua unakutana na changamoto nyingi sana ambzo unazipeleka mbele za Mungu kila siku kwa maombi sasa jifunze katika mwezi huu kuwa maombi pekee bila imani hayatengenezi jibu lako. Hivyo kwa kila unalo omba hakikisha umejumlisha na imani ndani yake nawe utaona jibu lako.


Na Patrick Sanga


No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...