Monday, July 9, 2012

Mch Mwaisumbe akemea Vikali mgomo wa Madaktari na waalimu nchini


KANISA  la Baptisti  Galilaya  Iringa limeeleza  kusikitishwa na migomo mbali mbali ya  wanatalum  ukiwemo  ule   madaktari  unaoendelea  hapa nchini kuwa  ni migomo yenye  lengo la  kuwatesa  watanzania  masikini na hivyo  kuwaomba  wanataluma hao   wakiwemo madaktari  na  walimu ambao  wametishia  kugoma kutanguliza  hofu ya  Mungu katika shughuli  zao na kuachana na mpango  huo kama njia ya  kumpunguzia mzigo wa mawazo Rais Jakaya  Kikwete.

Mch Mpeli Mwaisumbe

Mbali ya  kuwaomba  madaktari  kufanya kazi kwa  kutangulia  hofu ya Mungu na  kuwaonea  huruma  watanzania  wasio na  kipata  ambao ndio  wanateseka na migomo  hiyo bado  aliwataka  watanzania  zikiwemo  taasisi  za dini nchini  kuendelea  kumwombea afya  njema mwenyekiti  wa jumuiya ya  madaktari nchini Dkt Steven Ulimboka  na kuiombea  serikali ya  Rais Kikwete  ili  isiendelee  kuandamwa na  jinamizi  la migomo isiyo na  tija katika maendeleo ya  Taifa.

Kauli  hiyo  imetolewa jana na mchungaji  wa Kanisa  hilo  Mpeli Mwaisumbe(Pichani)  wakati  wa ibada maalum  ya kumsimika mchungaji mpya  wa kanisa  hilo   Hebron Mwakamwamba ibada  iliyomshirikisha  pia askofu  wa kanisa  hilo  Agripa Kyamajoli .


Alisema  kuwa  sifa  ya  amani ya  Tanzania  na upendo  imeanza  kutoweka  katika  kipindi  hiki  kutokana na wajuaji  kuwa  wengi na  watu ambao ni  tegemeo katika  Taifa   wakiendelea kugeuka kuwa  tishio  kwa  watanzania  wanyonge kwa  kutangaza  migomo mbali mbali  kwa ajili ya  kuangalia  maslahi  binafsi  zaidi badala ya  kuwasaidia   watanzania  wanyonge  kuweza  kunufaika na elimu zao.


Mwaisumbe  alisema  kuwa pamoja na  mazuri ambayo  Rais  kikwete  amekuwa akiyafanya  ila  kutokana na kuongezeka kwa matukio mengi ya  migomo ya  wanatalum ,Rais amejikuta  akiwa  katika mzigo mkubwa  wa  mawazo  kila  kukicha akiwaza ni wapi na kundi gani litaibuka na mgomo jambo ambalo wao kama kanisa  wanaona migomo kama  hiyo  inazidi kumtesa  Rais na hivyo kuna haja ya makundi  hayo ya  wanatalum  kujaribu kumfanya  Rais  kupumzika na  kushughulikia maendeleo ya  watanzania kwa ujumla badala ya  kila  wakati  kuzungumzia migomo ya madaktari na  walimu.

" Ndugu  zangu  waumini  hawa  madaktari na  walimu ni  waumini  wetu ambao  tumekuwa  tukisali nao kila jumapili na  watoto  wanaowafundisha na   wagonjwa  wanaowatibu madaktari  ni  miongoni  mwa  waumini  wa taasisi  zetu za dini na watanzania  wenzao ....sasa  leo  tunaposikia  daktari anagoma  kumtibu mgonjwa ambaye ni mlalahoi mwenzake ama  mwalimu anagoma  kufundisha   watoto  wetu ....kweli hawatutendei haki  sisi  watanzania  wanyonge hata kama  wana hoja  juu ya madai  yao  ila ni vema kutafuta njia nzuri isiyo mnyanyasa  mwingine  kwa  ajili  ya  kutafuta  ufumbuzi badala  ya  kukimbilia  kugoma .....naomba  sana wataalam wetu  wanapofanya kazi  zao watambue  kabisa  Mungu ndie anayewaongoza katika  shughuli zao  hivyo kabla ya kukimbilia  kugoma  basi  kutanguliza hofu ya Mungu ambaye amewapa uwezo wa kuwa katika nafasi hizo kuliko  kuwanyanyasa  watanzania " alisisitiza mchungaji Mwaisumbe

Kuwa mambo  saba katika Kanisa  la kwanza  yalikuwepo kwa  sasa  yameanza  kutoweka na  watu  kuanzisha mambo yao  wenyewe kwa  kuwatenda  vibaya  wengine huku  hata  baadhi ya nyumba  za ibada na  watumishi  kugeuza nyumba  hizo za ibada  kuwa ni sehemu ya  kutafutia utajili  binafsi ama kutafuta umarufu  wa  kisiasa badala ya  kuifanya kazi ya Mungu.

Dr Ulimboka akisalimiana na Waziri mkuu Mh Mizengo Pinda
" Leo  katika Makanisa  baadhi ya  wahubiri   wamekuwa  wakiingiza  siasa ya  Chadema ama  CCM na kutaka  kila jambo ambalo  wao  wanalitaka  lifanyike  lifanyike  hivyo ....nasema  watumishi  wenzangu tunalikosea kanisa na tunakwenda  kinyume na maandiko matakatifu  kwa  kuchanganya  siasa na dini katika nyumba  hizi  za ibada na ndio  sababu kila  kukicha Taifa  limekuwa  likiingia katika migomo na matukio ya ajabu ambayo awali hayakuwepo"

Hivyo  aliwataka  waumini  wa kanisa  hilo ambao ni  wasomi kuacha  kuingiza  usomi  wao katika  nyumba ya ibada na badala  yake  kutanguliza maombi kwa  kila jambo ili  kulisaidia Taifa   kuepukana na matukio ya migomo  isiyo  kuwa na kikomo inayoendelea  hapa nchini.

Mwaisumbe  aliwataka  waumini  wa kanisa  hilo  kuendelea  kuliombea  Taifa  la Tanzania  chini ya Rais Jakaya  Kikwete ,kuwaombea   wabunge na spika wa bunge  ili  bunge  liweze  kurejea katika misingi yake ya  kutunga sheria na kuwa ni chombo cha kuwawakilisha  wananchi badala ya  sasa chombo  hicho  kinavyotumika kama sehemu ya vijembe na malumbano  yasiyo na tija kwa  watanzania.

Huku  askofu  wa kanisa  hilo Agripa  Kyamajoli  akiwataka   watanzania  kuendelea  kumwombea afya njema Dkt  Ulimboka ili  apone na  kuja kuungana na  madaktari  wenzake  kuwatumikia  watanzania .

Pia  alitaka  mambo  zaidi  kwa kila mtanzania  kwa ajili ya  kukemea na kupambana na  watu  wanaojihusisha na matukio ya kinyama kama  hilo la Dkt  Ulimboka ili  washindwe na kuregea na kuachana na  vitendo hivyo  vya kinyama.

Na  Francis  Godwin

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...