Sunday, February 12, 2012

Maoni na ushauri wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania juu ya mgomo wa madaktari

Rais wa baraza la maaskofu wa katoriki nchini Askofu Mkuu Yuda Thadei Ruwa’ichi

Waona tukio la mgomo wa madaktari kama sehemu tulipoanguka kama taifa.

Wameitaka Serikali kuwa tayari kusikiliza madai ya watu na kuonyesha nia ya kufanyia suala la nyongeza za maslahi kwa makundi yote ya kijamii nchini bila kusuasua ili kuepusha uwezekano wa kuamsha hisia za uwepo wa matabaka miongoni mwa Watanzania.

BARAZA la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), limesema kauli ya Serikali kuwa haiwezi kutimiza madai yote ya madaktari kwa kisingizio cha mazingira magumu yanayoikabili, ni dalili ya kuanguka kwa taifa.TEC imesema utetezi huo wa Serikali hauna mashiko kwani yenyewe, imejaa  tuhuma za ubadhirifu na ufisadi.

Tamko la TEC kwa vyombo vya habari lililotolewa jana jumamosi na  kusainiwa na Rais wake, Askofu Mkuu Yuda Thadei Ruwa’ichi,  chini ya kichwa kisemacho , “Maoni na ushauri wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania juu ya mgomo wa madaktari”, lilisema madaktari ni kundi moja tu kati ya mengi yenye manung’uniko ya kuboreshewa mazingira ya kazi ndani ya jamii na kuishauri Serikali kutafakari na kuwa makini ili tukio hilo lisijirudie.

“Madaktari ni moja tu, kati ya makundi kadhaa ya wanajamii ambayo yamekuwa na madai na manung’uniko ya kuboreshewa maslahi au mazingira ya kazi.  Jibu la Serikali siku zote limekuwa ni kwamba hali ya uchumi ni ngumu na hivyo pamoja na nia njema, Serikali haina fedha za kushughulikia madai hayo,” ilisema sehemu ya tamko hilo na kuongeza:

“Kuna minong’ono na manung’uniko mengi ambayo hayapaswi kubezwa wala kupuuzwa kwamba kuna ubadhirifu na ufujaji wa rasilimali fedha katika baadhi ya sekta za umma jambo ambalo linaiweka Serikali katika wakati mgumu kuthibitisha kwamba haina fedha za kutosha kwa ajili ya kuboresha maslahi ya baadhi ya makundi ya wanajamii.” Maaskofu hao walisema tukio la  mgogoro wa Serikali na madaktari limeonesha udhaifu unaopaswa  kuepukwa katika siku za usoni.

"Hata hivyo sisi maaskofu tunaona tukio hili la mgomo wa madaktari kama sehemu tulipoanguka kama taifa. Hivyo hatuna budi kutafakari na kuona tulipojikwaa ili matukio kama hayo yasije kurudia tena katika nchi yetu na kushuhudia maafa kama tulivyoshuhudia,"ilieleza  sehemu ya tamko hilo.

Walisema hivi sasa ni muhimu kwa Serikali kuonyesha juhudi za makusudi, kuwasadikisha Watanzania kuwa kweli inakabiliwa na mazingira magumu ya kiuchumi sambamba na  kuongeza juhudi za kupambana na ufisadi, ubadhirifu na ufujaji wa mali ya umma.


Kauli hii ya TEC imekuja siku chache baada ya Serikali kumaliza mgomo wa madaktari kufuatia  Waziri Mkuu, Mizengo Pinda kukutana nao wiki hii  huku  akitangaza kuwasimamisha kazi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Blandina Nyoni na Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Deo Mtasiwa.

Vilevile, Serikali ilitangaza kupandisha posho za madaktari kutoka sh 10,000 kwa siku hadi sh 25,000  huku ikiahidi kuwapandishia mishahara na kuwapatia mikopo ya nyumba na magari.Maaskofu hao wameitaka Serikali kuwa tayari kusikiliza madai ya watu na kuonyesha nia ya kufanyia suala la nyongeza za maslahi kwa makundi yote ya kijamii nchini bila kusuasua ili kuepusha uwezekano wa kuamsha hisia za uwepo wa matabaka miongoni mwa Watanzania hali inayoweza kuzua  manung’uniko na kuamsha hasira kwa makundi mengine.

Kuhusu uwajibikaji wa viongozi na watendaji serikalini, TEC imependekeza uwepo wa ufuatiliaji wa karibu zaidi wa baadhi ya watendaji wakuu, taasisi hata Wizara za Serikali.
“Tunapendekeza uwepo ufuatiliaji wa karibu zaidi wa baadhi ya watendaji wakuu wa taasisi na hata wizara za Serikali,” tamko hilo la TEC lilieleza.

“Tunapendekeza kwamba kunapokuwa na migogoro na mivutano ya namna hiyo, itafutwe suluhu kwa kutumia upande watatu, badala ya kuwa na pande mbili zinazotunishiana misuli na kusababisha usumbufu, hofu, maumivu na maafa kwa raia wanyonge na wasio na hatia kama ilivyotokea katika mgogoro huu,” wameeleza maaskofu hao.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...