Saturday, June 25, 2011

Upendo Kilahiro: Nilikataa uraia wa Canada, Afrika Kusini

Upendo Kilahiro
Upendo Kilahiro ni Mtumishi wa Mungu ambaye Sanjari na mumewe, humtumikia Mungu kwa njia ya uimbaji. Awali kabla ya kuhamia rasmi jijini Dar es salaam kwa sababu za Kihuduma, kabla ya hapo alikaa na kuishi kwa muda mrefu jijini Arusha. Katika huduma yake ya uimbaji kuna kipindi alipata fursa ya kwenda nchini Afrika ya kusini. Akiwa huko, alikokaa kwa muda mrefu alifanikiwa kufanya huduma katika maeneo mbali bali ya nchi hiyo na aliweza kukubalika sana nchini humo.

Wakati wa harakati hizo za kihuduma wengi wa Raia wa Afrika ya kusini akiwemo mwanamama Rebeka Malope waliwahi kumuomba abadili uraia wa Tanzania na kuchukua uraia wa Afrika ya kusini ili aweze kufanya kazi zake kwa uhuru zaidi nchini humo lakini Upendo alikataa kata kata.

Kutokana na msimamo wake huo Malope alimuomba upendo kuwa msemaji wake katika ukanda wa Afrika Mashariki kazi anayoifanya mpaka sasa.  Hali  hiyo ilijitokeza tena alipokuwa ameenda nchini Canada Kihuduma., akiwa huko wenyeji wake na raia wengine nchini humo walimshauri vivyo hivyo lakini Upendo anasema “mimi niliwaambia kuwa ni Mtanzania na sitoweza kuisaliti nchi yangu hata kama ipo vipi”

Tofauti na uimbaji, Upendo Kilahiro amekuwa mstari wa mbele katika kuisaidia jamii ya watanzania wenye hali duni kimaisha na hii ilipelekea shirika la Afya ulimwenguni (WHO) kumchagua kama balozi wa shirika hilo nchini Tanzania kwa mwaka 2009.

Upendo kwa kushirikiana na Taasisi ya Christian Directory & Consultancy, alifanya tamasha kubwa la muziki wa Injili lililofanyika mkoani Arusha, lililokuwa na lengo la kuchangisha fedha za kuwasaidia wagonjwa wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, ambalo lilikwenda sanjari  na utambulisho wa Albamu yake iitwayo ‘Asante Yesu’

1 comment:

  1. Nawapenda na kuwaheshimu watu wanaoipenda Tanzania kwa dhati. Hivi kuna nchi nyingine nzuri kuliko Tanzania? Kamwe siwezi kuikataa Tanzania kwa kuibadilisha na nchi yoyote ile duniani. Congrats Upendo!

    ReplyDelete

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...