Thursday, November 8, 2012

Package from Altar:Ufunguo Wa Baraka Zako Kifedha




Malaki 3:1-12
Ule mstari wa nne na wa tano unasema “wakati ule ndipo dhabihu za Yuda na Yerusalemu zintakapopendeza mbele za Bwana, kama katika siku za kale, na kama katika miaka ya zamani nami nitawakaribieni ili kuhukumu; nami nitakuwa shahidi mwepesi juu ya wachawi, na juu wa wazinzi, na juu yao waapao kwa uongo; na juu yao wamwoneao mwenye kuajiriwa, kwa ajili ya mshahara wake, wamwoneao mjane na yatima, na kumpotosha mgeni asipate haki yake, wala hawaniogopi mimi, asema Bwana wa majeshi”

Mpenzi msomaji sijui kama unajua kwamba neno la Mungu ni jumla ya mawazo na majibu ya Mungu kwa mwanadamu. Kuna siri nyingi sana ndani ya Biblia, ambazo si rahisi kuzielewa mpaka Roho wa Yesu akufunulie kwa utukufu wake utakapomtafuta.
Ilikuwa tarehe 31/08/2008, wakati naomba nilimuuliza Mungu maswali mawili ya kifedha.  Moja lilihusu ujenzi wa kanisa la mahali ninapoabudu na la pili lilihusu mahitaji yangu ya kifedha.  Baada ya maombi hayo ndipo Mungu aliponifunulia siri hii nami nataka nikushirikishe. Ukiweka kwenye matendo siri hii naamini maisha yako ya kiuchumi yatabadilika na kuwa bora zaidi.

Inawezekana maisha yako kiuchumi kwa sasa si mazuri, biashara zako pia hazijakaa vema, miradi yako pia haijakaa vema ni kama haisongi mbele, kuomba unaomba, yumkini na fungu la kumi unajitahidi kutoa, na sehemu ya mapato yako unapeleka kwa watumishi, bado kuna fungu jingine hata maskini unawasaidia.
Huenda pia kama ni mwajiriwa selikarini au taasisi binafsi n.k unaona hautendewi haki katika malipo mbalimbali na hata mshahara wako pia.  Huenda wewe ni yatima au mjane halafu kuna haki zako ambazo zimetekwa na yule adui, huenda ni sehemu ya mirathi yenu, huenda kama wewe ni mjane basi stahili na mali ulizotafuta na mume wako zimechukuliwa na maisha ni magumu, unaona kama Mungu amekusahau na umeenda kwenye vyombo vya sheria lakini ufumbuzi bado haujapatikana nk.

Leo nina habari njema kwako, usidhani Mungu amekusahau, isipokuwa wewe ndio umemsahau, “Naam umemsahau”.  Mungu anachotaka ni kukupigania katika haki zako.  Mungu hafurahii unayoyapitia anataka upate haki zako zote.  Sasa ili uweze kupata haki zako ni lazima ujifunze na uanze kutoa dhabihu/sadaka za haki na za kumpendeza yeye.

Yawezekana pia baraka/haki zako  zimetekwa na wachawi, wazinzi, na watu waapao kwa uongo na wenye kukuonea. Wewe huna uwezo wa kuwashinda hawa watu kwa nguvu zako, naam  Mungu anao uwezo huo. Nguvu za Mungu za kukupigania na kurejesha baraka/haki zako zimo katika wewe kutoa sadaka za haki na za kumpendeza yeye.  i.e Kadri unavyotoa sadaka za haki ndivyo unavyomkaribisha  Mungu kukupigania na mbili ndivyo unavyowasogeza adui zako mbele za Mungu awashughulikie. Unamfanya Mungu asistarehe juu ya adui zako.
 
Mungu anposema  wachawi uwe na hakika anazungumzia watu ambao wanalenga kuharibu uchumi na mafanikio yako kwa ujumla katika kila nyanja  biashara,kikazi,kilimo, kiroho,kihuduma nk, na  anaposema wazinzi ana maana mbili moja ni hawa wazinzi/ makahaba wa kawaida ambao yumkini unatafuta fedha yako kwa jitihada lakini inaishia kwa hao na pili ni wale waganga wa kienyeji na watumishi/manabii wa uongo, wanaosema Bwana amesema toa hiki na kile utabarikiwa, huku mioyoni mwao wakijua hayo ni mawazo yao na si Bwana. 


Kibiblia huu ni  uzinifu wa rohoni. Yaani wamezini katika roho zao kwa kujifanya wana nena neno la Bwana kumbe ni mawazo yao.
Na anaposema waapao kwa uongo maana yake anazungumzia waongo kwa ujumla wanaweza kuwa washirika wako kibiashara, kikazi, kihuduma n.k watu wanaotumia uongo kukuibia pesa yako, muda wako, maendeleo yako wanaokopa wasilipe n.k Je kwa nini hayo yote yanakukuta wewe? . Ni kwa sababu bado hujatoa dhabihu za haki na za kumpendeza Mungu, naam bado hujatoa.

Je, Kutoa dhabihu za haki na za kumpendeza Mungu ndio kukoje?
Ni kutoa kwa muda na uongozi wa Mungu matoleo yako mbalimbali.  Si watu wengi wenye nidhamu hii. Pesa na utajiri ambao Mungu anakupa mkononi mwako ni kwa ajili ya kuimarisha agano lake pia.  Yaani kuhakikisha makusudi yake hapa duniani yanafanikiwa kwa kutumia watu anaowabariki.  Kumbuka kufanikiwa kwa makusudi ya Mungu duniani kunategemea utiifu wa watu wake duniani.   

Sasa hii ni pamoja na wewe kama mtu wa Mungu kutoa fedha yako kwa ajili kazi ya Mungu hapa duniani.
Suala sio kutoa tu, bali ni kutoa kwa kufuata muongozo wa Roho Mtakatifu ndani yako kwa maana ya wapi upeleke sadaka yako na pili kutoa kwa muda unaotakiwa kutoa kwa maana ya lini/wakati gani unatakiwa kutoa.
Jambo hili linaweza kuonekana gumu kwa jinsi ya kibinadamu, lakini huku ndiko kuongozwa na Roho Mtakatifu katika utoaji.  

Kama ukiweka mahusiano yako na Roho Mtakatifu kuwa mazuri ni rahisi sana kuona uongozi wake juu ya matoleo yako.  Fahamu kwamba baraka za mtaoaji zimefungwa katika muda na eneo/mahali anapotoa.  Hii ina maana kila sadaka unayotoa ina baraka zake.  Sasa baraka hizo zinategemeana na namna unavyotoa kwa maana ya muda na eneo.

Kwa hiyo jifunze kutoa kwa uongozi wa Mungu, kabla hujatoa sadaka yako, jifunze kumuuliza Mungu je sadaka hii napeleka wapi na kwa muda gani?     Kwa kufanya hivyo utakuwa umetengeneza mazingira ya Mungu kufungua baraza zako kifedha/kiuchumi n.k. Kama huoni baraka za Mungu kifedha kwako huenda ni kwa sababu umezizuia kwa kutotoa dhabihu (sadaka) za haki na za kumpendeza Mungu. Neno kumpendeza Mungu linawakilisha kiasi/kiwango na muda. Maana yake toa kwa kiwango anachotaka yeye kwa ajili ya kazi yake na si kwa kiwango unachotaka wewe na pili toa kwa muda anaotaka yeye na si wewe. Kinachosisitizwa hapa pia ni uaminifu katika kutoa na si kumuibia Mungu
(Malaki 3:8).

Na Patrick Sanga

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...