Tuesday, May 22, 2012

Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Edward Lowasa Anatarajiwa Kuwa Mgeni Rasmi Tamasha La Wezesha Upendo Radio



Waziri mkuu mstaafu mheshimiwa Edward Ngoyaine Lowasa anatarajiwa kuwa mgeni maalum katika tamasha la wezesha Upendo redio linalolenga kukusanya pesa za kitanzania zaidi ya milioni 220 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya kuboreshea na kuongeza usikivu wa matangazo ya redio hiyo litakalofanyika Mei 27 mwaka huu katika ukumbi wa Diamond Jubilee jijini Dar es salaam.

Akizungumzia juu ya tamasha hilo msaidizi wa askofu wa dayosisi ya mashariki na Pwani (DMP) wa  kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) mchungaji George Fupe amesema kanisa hilo limemtumia mwaliko mheshimiwa Lowasa kuwa mgeni maalum katika tamasha hilo kwani yeye ni mmoja wa washarika wa kanisa hilo.

Aidha mchungaji Fupe alisema  tayari wameshawatumia baadhi ya mawaziri,wabunge,wafanyabiashara,watu mashuhuri na viongozi mbalimbali wa serikali pamoja na wakuu wa dini na madhehebu mbalimbali waweze kushiriki baraka hizo.

Edward Ngoyaine Lowasa
"Tunawakaribisha si kwa sababu wamekuwa na nyasfa kubwa serikalini bali tumeangalia unyenyekevu wao kwa Mungu na kwa jamii"alisema mchungaji Fupe.

Aliongeza kuwa kwa taratibu za KKKT askofu wa dayosisi hiyo na ambaye pia ni askofu mkuu wa kanisa hilo hapa nchini Dr Alex Malasusa ndiye atakuwa mgeni rasmi katika tamasha hilo.

Alisema kuwa licha ya upendo redio kumilikiwa na kanisa hilo na hata kurusha vipindi vya dini pia imekuwa ikitangaza vipindi vingi vya kijamii kama vile vya ujasiriamali,wanawake na matumaini, walemavu,vijana,watoto,wazee,upendo mseto na hali halisi ambavyo vimekuwa msaada kwa jamii.

Tamasha hilo la aina yake litapambwa na vikundi mbalimbali vya kwaya pamoja na waimbaji  binafsi wa ndani na nje ya nchi  kama vile Faraja Ntaboba kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Sara Kimani kutoka nchini Kenya.

Wengine ni Jackson bent kutoka jijini  Arusha,Jennifa Mgendi kutoka jijini Dar es salaam na kwaya mbalimbali za KKKT Dayosisi ya Mashariki na Pwani (DMP).

Upendo redio Fm inayosikika katika masafa ya FM 107.7 Mhz ilianzishwa mwaka 2004 ikiwa chini ya DMP na inasikika mikoa saba hapa nchini ambayo ni Dar es salaam,Pwani,Morogoro,Tanga,Zanzibar na baadhi ya sehemu za mkoa wa Kilimanjaro lengo lake ni kutaka isikie ndani na nje ya nje

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...