Tuesday, October 30, 2012

Kanisa lajipanga kujenga Chuo jijini Mbeya



Jiji la Mbeya

UONGOZI wa Serikali mkoani Mbeya, umeliahidi Kanisa Katoliki Jimbo la Mbeya, kushughulikia ombi kulipatia eneo kwa ajili ujenzi wa Chuo cha Uuguzi katika Hospitali ya Igogwe, inayomilikiwa na kanisa hilo, wilayani Rungwe.

Kauli hiyo ilitolewa juzi na Mkuu wa Wilaya ya Rungwe, Chrispin Meela, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kndoro, alipokuwa akizungumza katika maadhimisho ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Hospitali ya Igogwe.
Meela alisema Serikali inalifanyia kazi  ombi la Askofu wa Jimbo la Kanisa Katoliki la  Mbeya, Evarist Chengula, kuhusu eneo lililo jirani na hospitali hiyo kwa ajili ya kuendeleza mipango ya uwekezaji.Mkuu huyo wa wilaya alisema kikwazo kilikuwa ni baadhi ya  wananchi  wanaomiliki eneo hilo, kukataa kuondoka.

Alisema kwa mujibu wa sheria za nchi, ardhi ni mali ya umma na kwamba aratibu za kisheria zinafanyika, ili kuona namna ya uwahamisha wakazi wa eneo hilo haraka iwezakanavyo.Meela alisema dhamira ya kanisa hilo ni kwa faida ya  umma wote wa Watanzania huku wakazi wa eneo hilo wakiwa walengwa wakuu .

“Kwa hiyo Serikali haitakubali kuona watu wachache wakizuia maendeleo ya Watanzania wengi. Nikuhakikishie tu baba Askofu Chengula kwamba maombi haya tuliyapata na sasa tumeanza kuyashughulikia ipasavyo kwa kuangalia namna ya kuwahamisha watu wote wanaomiliki ardhi hiyo ili muweze kuanza kazi yenu ya ujenzi wa chuo hicho kwa faida ya wanarungwe na Watanzania kwa jumla wake,” alisema Meela.

Hospitali ya Igogwe ilianzishwa na watawa kikatoliki kutoka Holand mwaka 1962  na mwaka huu ilikuwa ikiadhimisha Jubilei ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwake.
Mapema katika hotuba yake, Askofu Chengula alisema ni muda mrefu tangu kanisa katoliki lilipofikisha maombi yake serikalini kuomba lipewe eneo hilo kwa ajili ya ujenzi wa chuo cha uuguzi, lakini ombi hilo limekuwa halijibiwi.

Alisema licha ya kutengwa kwa  fedha za ujenzi wa chuo na kuwapo kwa   wafadhili wa kusaidia mradi huo, kikwazo kimekuwa ni upatikanaji wa eneo hilo.Alisema kama kanisa hlitafanikiwa kupata eneo la kujenga chuo hicho, litasaidia kusomesha watalaamu wa afya si kwa hospitali zake pekee, lakini pia hata za Serikali na  hivyo kupunguza tatizo la uhaba wa watalaamu wa afya nchini.

Source: Mwananchi

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...